Mkuu wa majeshi ya Ulinzi nchini Uganda Jenerali Muhoozi siku ya Jumatatu alijisifu kwa kupanga kumsababishia “maumivu na uchungu” mwanasiasa wa upinzani ambaye amemkamata, aliyekuwa akijiandaa kuwasilisha pingamizi la kisheria dhidi yake.
Muhoozi Kainerugaba, mwana wa Rais aliyetawala kwa muda mrefu Yoweri Museveni, alichapisha picha kwenye mtandao wa X ya Erias Lukwago, mwanasiasa wa upinzani na wakili anayeshikiliwa na jeshi.
“Ninajivunia maumivu na uchungu WOTE nitakaoupata kwa LUKWAGO MHALIFU!” Kainerugaba alichapisha ujumbe huo kwa wafuasi wake milioni 1.3 kwenye mtandao wa X.
“Anaendelea kusema ‘Samahani, samahani’. Haitamsaidia kwa sasa,” aliandika kando ya picha ya Lukwago, akiwa amevaa fulana nyeupe.
Picha nyingine inaonyesha mwanamume aliyevaa nguo kama hiyo, kwenye mandhari kama hayo hayo, uso wake ukiwa umefunikwa kwa kitambaa na mikono ikiwa imeunganishwa kana kwamba anaomba dua.
Katika chapisho la awali kwenye mtandao wa X, Kainerugaba alisema “alimkamata mjinga na kumpeleka kwenye chumba cha chini ya ardhi”, lakini hakumtaja Lukwago.
Aliandika katika chapisho lingine: “aliniita?? Unathubutuje kutamka maneno hayo”, akiongeza: “mpumbavu huyu atajifunza kutokana na makosa yake”.
