

Klabu ya Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini imetangaza kumsajili kiungo mkabaji wa Tanzania, Adolf Mtasingwa Bitegeko, kutoka Azam FC kwa ada ambayo haijawekwa wazi baada ya pande zote mbili kufikia makubaliano.
Mtasingwa mwenye umri wa miaka 27, ambaye alikuwa nahodha wa Azam FC, anakuwa mchezaji wa kwanza kutoka Tanzania kujiunga na Kaizer Chiefs. Usajili wake unaongeza orodha ya wachezaji kutoka zaidi ya mataifa 20 ya Afrika waliowahi kuvaa jezi maarufu ya dhahabu na nyeusi ya klabu hiyo.
Kiungo huyo wa kimataifa wa Tanzania anakuja na uzoefu mkubwa baada ya kucheza kwa misimu sita katika ligi za Scandinavia, akishiriki kwenye ligi za Iceland, Norway na Finland kabla ya kurejea nchini mwaka 2024 na kusaidia Azam FC kumaliza nafasi ya tatu kwenye Ligi Kuu Tanzania msimu uliopita.

