
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema kuwa mauzo ya nyama nje ya nchi yameongezeka kutoka tani 1,774 mwaka 2020/2021 hadi kufikia tani 14,701 mwaka 2022/2023.
Amesema hatua hiyo imechangiwa na ushirikiano wa kibiashara na mataifa mbalimbali duniani uliohamasishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Amesema hayo leo Jumatatu (Mei 13, 2024) wakati wa hafla ya uzinduzi na makabidhiano ya Kituo Atamizi cha Ufugaji wa Kibiashara kwa Vijana kilichopo Kongwa mkoani Dodoma. Kituo hicho ambacho ni maalum kwa ajili ya unenepeshaji wa mbuzi kimegharimu sh. bilioni 1.6.
“Masoko ya nyama yameendelea kuongezeka na kuzifikia nchi 12 ambazo ni Bahrain, Comoro, Hong Kong, Jordan, Kenya, Kuwait, Oman, Qatar, Rwanda, Saudi Arabia, UAE na Vietnam.”


